SERIKALI
 ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) imesema operesheni ya kuwasaka wahalifu 
walihusika na vurugu za wiki iiliyopita inaendelea na Serikali haitakuwa
 na msalia mtume kwa yeyote aliyehusika na vurugu hizo.
Akizungumza
 katika mkutano na viongozi wa dini katika ukumbi wa Kanisa la 
Pentekoste Tanzania lililopo Kariakoo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa
 Pili wa Rais, Mohammed Aboud Mohammed alisema Serikali imesikitishwa na
 kitendo kilichotokea cha vurugu na uchomaji wa nyumba za ibada, 
Makanisa.
“Hizi
 ni njama za makusudi, nataka nisemawazi kwamba watu hawa wametangaza 
mapambano na Serikali,tutawashughulikia ipasavyo,” alionya Waziri Aboud.
Watu waliofanya vurugu Zanzibar sasa watakiona kwani wametangaza mapambano na Serikali, itawashughuliki popote walipo.
Waziri
 Aboud alisema kwamba waumini wa dini zote wamekuwa wakiishi kwa upendo 
na maelewano makubwa kwa miaka mingi ambapo ustahamilivu wa kidini upo 
kwa hali ya juu katika Visiwa vya Unguja na Pemba.
“Mie
 nakumbuka nilipokuwa nakaa kule Shangani kwa mfano Mwezi wa Ramadhani 
utakuta tunapelekeana vyakula, waislamu wanapeleka kwa wakristo na hata 
siku ya sikuuu ya Idd el Fitr tunasherehekea pamoja, huwezi kubagua yupi
 mkristo yupi Muislam,” alisema waziri hyo.
Alisema
 Serikali inawapo pole waumini wa makanisa yaliyochomwa moto na 
kuwaahidi hatua kali zitachukuliwa dhidi ya wale wote waliohusika.
Akizungumza
 katika mkutano huo,Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali Said 
Mwema alisema Polisi imejipanga kimkakati kukabuiliana na wale wote 
watakaofanya au kuchochea ghasia.
“Tunaendelea
 kudhibiti hali,doria kama kawaida na pia tumeweka ulinzi maalum katika 
nyumba za ibada tumezijumuisha katika sehemu muhimu za ulinzi kwa 
kipindi hichi,” alisema IGP Mwema.
IGP
 Mwema alisema pia ameunda timu maalum ya kikosi kazi ambacho 
kinajumuisha maafisa kutoka Idara ya Upelelezi Makao Makuu Dar es Salaam
 kuchunguza matukio ya vurugu hizo na kuwachukulia hatua watakaobainika.
Alisema
 katika mkutano huo pia jumla ya watu 46 wamekamatwa jana (juzi) na kati
 ya hao 43 wamefikishwa  mahakamani jana Mjini Zanzibar wakikabiliwa na 
tuhuma mbalimbali.
Kwa
 upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Abdallah Mwinyi 
Khamis alisema Serikali ya Mkoa wake imesikitishwa mno na vitendo vya 
ghasia na uchomaji wa makanisa moto.
Mkuu
 huyo wa Mkoa alisema uvumilivu wa kidini ni jambo la msingi sana na 
anaamini waliofanya vurugu na kuchoma baadhi ya makanisa moto sio 
waumini wa dini ya Kiislamu bali ni wahalifu.
“Tujiulize
 jamani, hivi kweli muumini wa kiislam anaweza kwenda kuvunja baa na 
kasha kuanza kunywa pombe? Hawa sio Waislam …hapa kuna jambo, 
tutawachunguza kubaini chanzo na wanaohusika na kadhiaa hii,” alisema 
Mkuu huyo wa Mkoa.
Akithibitisha
 uvumilivu wa kidini uliokuwepo Zanzibar tangu enzi na enzi, Mkuu wa 
Mkoa alitoa Stempu ya Serikali ya Kikoloni iliyopambwa kwa picha za 
misikiti na makanisa wakati wa utawala wa Kisultani chini ya himaya ya 
Uingereza yenye ujumbe wa uvumilivu wa kidini Zanzibar.
“Stempu
 hii iliyokuwa imetolewa na Serikali ya Kiingereza wakati ule 
inathibitisha kwamba Zanzibar hakuna tatizo la waislamu na wakristo,huu 
jamani ni ushahidi tunashangaa leo wanatoka watu wanachoma moto kanisa,”
 alisema.
Alitoa
 mfano wa namna wananchi Zanzibar walivyokuwa wakiishi kwa upendo na 
mshikamano wa maziko ya aliyekuwa Waziri Mwandamizi katika Serikali ya 
Mapinduzi Zanzibar, marehemu Brigedia Jenerali Adam Mwakanjuki, idadi ya
 Waislamu mazikoni ilikuwa kubwa kuliko ya dini nyingine.
“Mbali
 na hili la mwenzetu Mwakanjuki, mimi mwenyewe niliombwa na Skuli ya 
Kanisa St Joseph kusomesha, walikuwa na upungufu wa walimu, Wizara ya 
Elimu ikaniteuwa mie nienda kusomesha, nimeishi nao vizuri, 
hawakunitenga …mimi ndio mwalimu wa mwanzo muislam kusomesha skuli ya 
wakristo hapa Zanzibar,” aliongeza Mkuu huyo wa Mkoa.
Katibu
 Mkuu wa Makanisa ya Pentekoste Tanzania, Askofu David Mwasota 
aliishukuru Serikali kwa  kuwaunga mkono na kuwa pamoja nao kitendo 
ambacho kinathibitisha dhamira njema ya Serikali na viongozi kwa ujumla.
Askofu
 Mwasota alisema kesho (leo) watafanya mkutano wa madhehebu yote ya 
kidini kuzungumzia kadhia hiyo mkutano ambao utafanyika katika Kanisa la
 Pentekoste Kariakoo Unguja.
Mkuu
 wa Dini ya Kiislam katika Ofisi ya Mufti Mkuu Zanzibar, SheikhThabit 
Noman Jongo ameshangazwa na watu wanaochoma moto makanisa na 
kuwafananisha watu hao kuwa ni wahalifu na Serikali iwachukuli hatua 
kali kwani Waislam hawana ugomvi na Wakristo.
 
 Na Juma Mohammed – MAELEZO, Zanzibar