0diggsdigg
SERIKALI imekiri kuwa hali yake kifedha ni mbaya, ndiyo maana halmashauri nchini hazina fedha za kuendesha mambo mbalimbali ya kiutendaji.Desemba 6 mwaka jana gazeti hili liliripoti kwamba Serikali inakabiliwa na ukata uliosababisha wizara, idara na taasisi za Serikali zikiwamo baadhi ya vyuo vyake vikuu, kushindwa kufanya baadhi ya kazi zake, lakini Serikali ilikanusha. Jana, Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Mkuchika alipokuwa akijibu swali la mbunge wa Singida Magharibi, Mohammed Missanga alikiri ukata huo na kueleza kuwa ni tatizo kubwa. Missanga alitaka kupata kauli ya Serikali kuhusu ukata uliozikumba halmashauri nchini kwa kukosa fedha kutoka Serikali Kuu, kitendo ambacho kimesababisha zishindwe kufanya mambo mbalimbali ya kiutendaji ikiwamo kuendesha vikao vyake na kusimamia maendeleo ya miradi. Akijibu swali hilo, Mkuchika alisema halmashauri zina tatizo kubwa la fedha ambalo linasababisha baadhi ya mambo ikiwemo kufanyika kwa vikao vya kiutendaji kusimama. Aliongeza 'Kiwango cha fedha ni kidogo na hili liko mikononi mwa Waziri Mkuu." Alisema tatizo hilo ni kubwa mpaka Chama cha Serikali za Mitaa (ALAT) kimeomba kukutana na uongozi wa juu wa Serikali, ili kuzungumzia tatizo hilo. Mkuchika alisema katika halmashauri zote nchini hivi sasa kuna matatizo makubwa yanayotokana na ukata wa fedha ambazo kwa muda mrefu hazijapelekwa huko, huku akikiri pia hata fedha za mwaka jana hazijapatikana. Katika kuthibitisha tatizo hilo, Waziri huyo pia alishindwa kueleza lini fedha hizo zitapatikana na kupelekwa kwenye halmashauri. “Hata za mwaka jana hatujapeleka huko ndio maana wanalalamika, hata ALAT wameomba kukutana na uongozi wa juu serikalini kuzungumzia jambo hilo, lakini, kwa ujumla hali ni mbaya,’’alisema Mkuchika. Ukata huo ulisababisha kuchelewa kwa ruzuku ya vyama vya siasa vyenye wabunge na madiwani, hali iliyoathiri uendeshaji wa shughuli za ndani za vyama hivyo kikiwamo chama tawala, CCM. Akizungumzia hali hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa(LAAC), Augustino Mrema alisema ukata huo umesababisha miradi mingi kukwama kutokana na bajeti iliyopitishwa kutotekelezeka. Alisema ni kweli Serikali inayumba kwa kuwa hali ya fedha ni mbaya. "Alichosema Mkuchika ni sahihi na nampongeza kwa kukiri kuwa hawana fedha kwa kuwa mambo hayaendi kabisa huko kwenye halmashauri." Mrema aliongeza, "Kwa mfano kule Himo waliniambia wangenipa Sh150m kwa ajili ya mradi wa maji, lakini hadi hivi sasa wametoa Sh50 milioni ambazo haziwezi kufanikisha mradi huo." mwananchi |

Majaji katika mahakama ya ICTR
Mahakama inayoendesha kesi za
mauaji ya kimbari yaliyotokea Rwanda mwaka 1994 imetoa wito kwa mataifa
kutoa hifadhi kwa wale walioondolewa mashtaka.
Watu 5 kati ya watu 10 walioondolewa lawama za kuhusishwa katika mauaji hayo wanasema hawawezi kurejea nchini Rwanda.Wanaishi chini ya ulinzi wa Polisi katika nyumba moja mjini Arusha, Tanzania, ambako ndiko makao ya mahakama hiyo ya ICTR.
Mahakama hiyo ya ICTR inatarajiwa kufunga mwishoni mwa mwaka huu.
Watu 800,000 kutoka jamii ya waTutsis na waHutus wenye msimamo wa kadiri waliuwawa katika kipindi cha siku 100 nchini Rwanda mwaka 1994.
Msemaji wa ICTR Roland Amoussouga ameambia BBC kupatikana nchi za kuwahifadhi wale ambao hawakupatikana na hatia ndio changamoto kuu inayokabili mahakama.
"Ni mzigo mkubwa kwetu kuendelea kuwahifadhi watu hawa walioachiwa huru kwa muda wa miaka mingi hivi, na tumeshirikiana nao, pamoja na mawakili wao kutafuta nchi ambako wanaweza kupelekwa. Hadi sasa hatujafanikiwa," alisema.
Wote 5 walioko mjini Arusha ni kutoka kabila la waHutu na miongoni mwao ni afisa wa zamani wa jeshi wa cheo cha Brigadier generali, mawaziri wa zamani na mfanya biashara mmoja.
Wanaishi pamoja katika nyumba inayolindwa, wanaweza kwenda mjini na kanisani, lakini hawawezi kuondoka huko.
Waziri wa zamani wa uchukuzi Andre Ntagerura amekuwa akisubiri kupata hifadhi kwa kipindi cha miaka 6 tangu mashtaka dhidi yake yalipoondolewa.
Wengine wawili wameshatumika vifungo vyao lakini hawana pa kwenda.
Wote wana familia nchini Ubelgiji, Canada na Ufaransa lakini hadi sasa hawawezi kupewa vibali kujiunga na familia zao, licha ya maombi kutoka baraza la usalama la umoja wa mataifa.
bbcswahili