Saturday 14 September 2013

Padri amwagiwa tindikali Zanzibar




Sept 14, 2013:

Padri wa Kanisa la Romani Katoliki Parokia ya Machui, Joseph Monesmo Magamba amemwagiwa tindikali na watu wasiojulikana katika Mtaa wa Mlandege jana jioni, Mkoa wa Mjini Magharibi, Zanzibar.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Haji Hana alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba kiongozi huyo wa dini amelazwa katika Hospitali ya Mnazi Mmoja, akiendelea na matibabu baada ya kujeruhiwa usoni, kifuani na mikononi.

Hana alisema kwamba Padri Magamba (60) alikuwa akitokea katika duka la huduma za mawasiliano ya mtandao la Shine Shine saa 10.15 jioni na watu waliommwagia walimtega mlangoni kabla ya kufanya uhalifu huo na kutoweka kwenye vichochoro vya Mitaa ya Mtendeni na Mchangani.

Alisema polisi wamestushwa na tukio hilo kwa vile limetanguliwa na matukio matatu ya kumwagiwa tindikali kwa viongozi wa dini na kuwataka wananchi kutoa ushirikiano wa kufanikisha kuwakamata watu wanaojihusisha na vitendo hivyo.

“Tumeanza kufanya uchunguzi ikiwemo kuchukua maelezo ya majeruhi, tungependa zaidi kupata msaada wa kitaarifa kwa watu walioona na wanaojua mahali walipo watu wanaofanya vitendo hivyo,” alisema Hana.

Mfanyakazi wa Duka la Huduma za Mawasiliano ya Mtandao, Rukia Yahya Abass alisema anamtambua Padri Magamba kama mteja wake wa muda mrefu na huja dukani hapo nyakati za asubuhi au jioni kwa ajili kupata huduma za mawasiliano.

Rukia alisema ameshtushwa kuona padri huyo baada ya kumaliza kupata huduma na kutoka nje akipiga mayowe ya kujeruhiwa.

“Nimezoea kumwita father au babu, ni mteja wangu kwa kweli, nilimwona akirudi tena ndani huku akiomba msaada, watu waliokuwa katika mtandao harakahara wakammwagia maji, alikuwa akilalamika kwa ukali wa maumivu,” alisema Rukia akiwa na huzuni.

Alisema wasamaria wema ndiyo waliomchukua na kumpeleka hospitali. Kabla ya tukio hilo alilipa gharama za huduma ambazo zilikuwa ni Sh2,000 na kurudishiwa chenji yake baada ya kutoa noti ya Sh10,000.

Daktari Jamal Adam ambaye pia ni Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Mnazi Mmoja alisema kwamba Padri Magamba amepatiwa huduma ya kwanza na anaonekana amejeruhiwa usoni, mikononi na kifuani.

“Ni mapema mno kusema ameathirika kwa kiasi gani kutokana na tukio hilo, tunaendelea na juhudi za kumtibu, ”alisema Dk Jamal.

Huu ni mfululizo wa visa vipatavyo vinne vya kikatili ambavyo vimefanyika Zanzibar, vikiwalenga watu maalumu katika kipindi cha miezi 10 iliyopita.

Desemba mwaka jana, watu ambao bado hawajafahamika wamlipiga risasi Padri Ambros Mkenda wa Kanisa Katoliki la Mpendae mjini Zanzibar na kumjeruhi vibaya.

Februari mwaka huu aliuawa kwa kupigwa risasi kichwani, Padri Evarist Mushi wa Kanisa Katoliki katika eneo la Mtoni, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Agosti mwaka huu wasichana wawili, raia wa Uingereza waliokuwa walimu wa kujitolea, walimwagiwa tindikali na kujeruhiwa kifuani, shingo na uso.

No comments:

Post a Comment