Saturday 14 January 2012

UTABIRI WA MWAKA 2012


mrithi wa kazi za SHEIKH YAHYA Maalim Hassan Yahya Hussein amechukua nafasi yake na kufanya utabiri ambao umesambazwa katika vyombo vya habari kama ifuatavyo:
Mwaka 2011 ulianzia siku ya Jumamosi ambayo inatawaliwa na Sayari ya Zohal na Nyota zake ni Mbuzi na Ndoo. Sayari hii Nyeusi na inahusika na mambo mabaya,  kama vile ndoa kuvunjika, vita, kuvunjika kwa vitu au kuanguka kwa Serikali, fitina, magomvi, vifo vya waandishi na watu maarufu, shida nyingi, maradhi mengi, hujuma, kuongezeka kwa hofu  mabalaa kwa wasafiri wa bara na baharini, mvua kubwa  maafa na majanga ya asili.
 Katika utabiri wake alioutoa Februari mwaka jana miezi mitatu kabla hajafariki aliyekuwa Bingwa wa Utabiri hapa nchini Marehemu Sheikh Yahya Hussein alielezea mambo mengi kuhusiana na hayo  na mengi sana yametokea na bado yanaendela kutokea,  kubwa kabisa ni kuanguka kwa Serikali kadhaa za Kiarabu, na kukimbia kwa viongozi wa nchi za Tunisia na Misri, kuuwawa kwa kiongozi wa Libya Kanali Muamar Gaddafi, kiongozi wa Yemen kupata matatizo na mpaka hivi sasa Syria bado kuna matatizo.
Alitabiri pia  majanga ya asili na maafa kutokea sehemu mbali mbali za dunia, vifo vya Waandishi wa habari ambao mpaka sasa waliofariki na wanaofahamika hapa kwetu ni
  1. Hassan Mgenyi
  2. Juma Penza
  3. Dan Mwakiteleko
  4. David Wakati
  5. Maulid Hamad Maulid
  6. Adam Lusekelo
  7. Joseph  Kaitani Asama
  8. Alfred Ngatezi
  9. Halima Mchuka
  10. John Ngahyoma
  11. Mwinyimvua  Ahmed
Vile vile alitabiri kuhusu majanga kwa  wasafiri wa bara yaani nchi kavu na baharini na tumeona maafa ya kuzama kwa meli ya Mv Spice Islander,   na ajali zilikuwa nyingi.
Alitabiri pia kutokea kwa  Mafuriko sehemu mbali mbali za dunia na mpaka hapa kwetu  Dar es Slaam tulikumbwa na mafuriko ambayo yamesababisha vifo vya Watanzania zaidi ya 40 na matabiri mengine mengi ambayo hatujayaorodhesha yalitokea.
Kwa ujumla mengi aliyoyatabiri kutokea katika mwaka 2011 yametokea na mengine yanaendela kutokea mpaka Mwaka wa kinyota utakapomalizika mnamo Machi 20, mwaka huu (2012).
Mwaka huu wa 2012 umeanzia siku ya Jumapili, siku hii inatawaliwa na Sayari ya Jua ambayo nyota yake ni moja tu nayo ni nyota ya Simba.
Sayari hii inahusika na, kufanyiana kiburi, kutumia nguvu, ufahari, mambo yote yanayohusiana na Siasa, udereva, ufundi wa mambo ya moto na magari
Tarehe  20/5/2012 ambayo pia itakuwa siku ya Jumapili Jua litapatwa kiasi (Partial Eclipse) kwa mara ya kwanza na kupatwa huku kwa jua kutaonekana kwa upana wa kati ya kilometa 240 na 300 na sehemu zitakazohusika ni Asia Mashariki, Kaskazini mwa bahari ya Pacific na Magharibi ya Marekani.
Tokyo (Japani) ambayo iko kilometa 10 mwa mstari wa kati itashuhudia kupatwa huku kwa dakika 5 na sekunde 26.
Mwisho wa Mwaka huu tarehe 13/11/2012 ambayo itakuwa siku ya Jumatano ambayo inatawaliwa na sayari Mercury jua litapatwa kamili (Total Eclipse)  watu wanaoishi Australia na Bahari ya Pacific ndio watakaokumbwa na kiza cha kupatwa na jua. 
Kwa sababu huu mwaka umeanzia na siku ya Jumapili na siku hiyo inatawaliwa na sayari ya Jua, hatari za kupatwa huku zitaikumba Dunia moja kwa moja.
Mwaka huu una namba 12  (2012) ambayo kinyota inaashiria, uadui wa kisiasa na kijamii, watu kulipizana visasi na upinzani kupata nguvu, wanyonge kudai haki zao kwa nguvu na mafanikio ya wataliwa dhidi ya watawala.
Vile vile inaashiria kutokea kwa vimbunga, kusikika sana kwa habari za Waandishi au Waandishi kupata madaraka makubwa katika siasa.
Pia ni mwaka ambao kutazuka  Moto sehemu mbalimbali duniani na kuleta madhara makubwa na hiyo inaashiria kuzuka kwa magomvi  baina ya viongozi wa kisiasa na wananchi.
Pamoja na hayo tutasikia habari za kutokea matetemeko ya ardhi yatakayoleta madhara makubwa, Wasanii kupata kwa kuchaguliwa au kuteuliwa kushika nafasi za kisiasa na kutokea kashfa kubwa kwa viongozi zitakazohusiana na masuala ya fedha au mambo ya ufisadi au wizi mkubwa utakaoshitua watu.
Kutokana na hayo:-
Natabiri kutokea shida kubwa za Majanga ya Asili na kuongezeka kwa maradhi au kufumuka maradhi yasiyojulikana na kuiletea Dunia wasiwasi mkubwa.
Natabiri, Uadui mkubwa kutokea kati  ya viongozi wa nchi na wananchi kwa ujumla na kusababisha vita vya wenyewe kwa wenyewe  na viongozi kuvuliwa madaraka.
Natabiri kutokea vifo vya Mahakimu na Majaji na Wanasheria maarufu katika nchi za Mashariki, Tanzania ikiwemo
Natabiri kutokea vifo vya Mawaziri na Wizara zao kupatwa na matatizo.
Natabiri  Kutokea kwa Njaa kali kutokana na Jua kuwa kali na ukame kukumba nchi.
Natabiri tutasikika habari za wanawake kuuwa waume zao na watumishi kuwauwa mabwana wanaowafanyia kazi.
Natabiri Mwaka huu ni mwaka ambao utatawaliwa na vifo vitakavyoshtua watu wengi.
Natabiri:  Huu ni mwaka wa vijana kushika nafasi za uongozi na kuchukua madaraka na wazee wengi watapoteza nafasi zako hasa katika chaguzi mbali mbali zitazofanyika.
Natabiri malumbano makubwa, vurugu na magomvi kwenye mabunge, wabunge watagombana  bila kujali itikadi za vyama vyao.
Natabiri mivutano iliyopo hivi sasa katika vyama haitaharibu vyama husika hasa katika vyama vya CUF,NCCR na CCM.
Natabiri: Kutokea vifo vya ghafla kwa viongozi  wa kisiasa waliopo madarakani au Serikalini.
Nashauri:-  Serikali iwe makini katika utekelezaji wa shughuli zake kwa sababu kunaweza kuzuka mgogoro mkubwa utakaotikisa nchi.
Natabiri, Rais Jakaya Kikwete kupata umaarufu mkubwa wa kisiasa mwaka huu na atashirikisha wapinzani katika shughuli kadhaa za kiserikali hivyo nyota yake kuzidi kung’aa kitaifa.
Natabiri baadhi ya viongozi wa dini kukumbwa na kashfa mbaya na za kutisha zitakazovunja hadhi zao.
Maalim Hassan Yahya Hussein
S.L.P  21250 Simu 0754672464

1 comment:

  1. eheeeeee! huyo ni shekh yahya namba 2 jamani

    ReplyDelete