Wednesday 14 March 2012

AUNT LULU NA ULEVI


Na Erick Evarist
AMA kweli sikio la kufa halisikii dawa! Msemo huo umethibitika baada ya aliyekuwa Mtangazaji wa Runinga ya C2C, Lulu Semagongo ‘Anti Lulu’ kukutwa akiwa amelewa tilalila, siku chache baada ya kuahidi kuachana na tabia zisizofaa ikiwemo ya ulevi, Risasi Mchanganyiko linaripoti kifua mbele.
HABARI KAMILI
Tukio la Anti Lulu kulewa na kuzima kisha kujiachia mikao ya kihasarahasara lilishuhudiwa laivu na paparazi wetu, wikiendi iliyopita katika Viwanja vya Leaders Club, Kinondoni, Dar.
Kwa muda mrefu, kamera yetu ilimuumilika tangu alipoanza kupoteza muelekeo, lakini aliendelea kugigida ulabu, kiasi cha kufikia hatua ya kukaa chini kwa uchovu wa kilevi (angalia picha ukurasa wa nyuma).
Risasi Mchanganyiko likawa na kazi ya kwanza, ambayo ni kumfotoa picha za fasta na kujiwekea ushahidi kibindoni kabla ya kuelekea katika hatua ya pili.

WADAU WAFUNGUKA
Baada ya kupata picha zake za kutosha, mwandishi wetu aliwafuata baadhi ya wadau waliokuwa karibu naye na kuzungumza nao juu ya hali ya Anti Lulu.
“Alikuwa na rafiki zake, alivyoanza kulewa wakamzuia kuendelea kunywa lakini mwenyewe akakataa. Huyu mtoto nakwambia ni sikio la kufa. Hawezekani huyu,” alisema dada mmoja aliyejitambulisha kwa jina moja la Mayunga.
Husna Shaban aliyekuwa eneo hilo alipotakiwa kutoa maoni yake alisema: “Juzi tu nilisoma kwenye gazeti, akijishaua kuwa eti amebadilika na ataacha ulevi, yako wapi sasa? Ona alivyokaa hovyo, wahuni wanaweza kumfanyia lolote akiwa katika hali hiyo. Anatakiwa kubadilika.”

TUJIKUMBUSHE
Matoleo kadhaa yaliyopita, katika gazeti hili, Anti Lulu aliandikiwa barua na mwandishi wa safu hiyo Joseph Shaluwa, ikimtaka abadilishe mienendo yake ikiwa ni pamoja na kuacha kuvaa mavazi ya nusu utupu na ulevi wa kupindukia.
Katika toleo lililofuata, gazeti hili liliandika habari iliyokuwa na malalamiko kutoka kwa ndugu zake akiwemo mama yake mzazi juu ya tabia zake; alipopatikana kwa njia ya simu, Anti Lulu alisema atafuata ushauri wa barua hiyo na kuwaomba radhi wazazi wake.
Ikiwa hata wiki sita hazijakatika, tayari amerudi kule kule na hivyo kuthibitisha kwamba hawezi kubadilika na ahadi aliyoitoa kwa ndugu zake ilikuwa danganya toto.

YEYE ANASEMAJE?
Siku ya tukio, mwandishi wetu hakufanikiwa kuzungumza naye kutokana na hali ya ulevi aliyokuwa nayo, lakini alipopatikana siku ya pili yake aliruka kimanga.
“Mimi nilikuwa Leaders? Aah! Jamani, mbona nimeshaacha mambo hayo siku hizi? Aliyewapa hiyo habari amewaongopea,” alisema bila aibu akiwa hajui kuwa kuna ushahidi wa kutosha.

KALAMU YA MHARIRI
Kuna msemo unasema, asiyefunzwa na mamaye hufuzwa na ulimwengu. Anti Lulu anapaswa kujua kwamba yeye ni kioo cha jamii na tabia zake zinaweza kumporomosha mara moja.

chanzo:GPL

No comments:

Post a Comment