Saturday 19 January 2013

Mawaziri waibua madudu ya kutisha bandarini Dar



Kaimu MKurugenzi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) Madeni Kipande (Kulia) akitoa maelezo kwa Mawaziri waliotembelea uongozi wa TPA ili kufahamu matatizo na changamoto zake jijini dar es Salaam jana, kutoka kushoto ni Waziri wa Fedha Dk William Mgimwa , Waziri wa Uchukuzi Dk Harrison  Mwakyembe na  Waziri wa Viwanda na Biashara Dk Abdallah Kigoda  Mwananchi

MAWAZIRI wanne wa Serikali ya Rais Jakaya Kikwete wameipa siku mbili Bodi na Menejimenti ya Mamlaka ya Bandari (TPA) kueleza sababu za kubadilishwa kwa kipengele cha mkataba wa ujenzi wa Mtambo wa Kupakua Mafuta katika Meli (SPM) bandarini.
Kutokana na kubadilishwa kwa kipengele hicho, TPA italazimika kutoa kiasi cha Dola 3 milioni ambazo ni sawa na takriban Sh4.8 bilioni katika kipindi cha miaka miwili kwa ajili ya kukarabati mtambo huo.
Pia wameagiza moja ya mashine inayotumika kukagua mizigo inayoingia katika bandari hiyo, iliyopelekwa katika Bandari ya Tanga miaka miwili iliyopita irejeshwe mara moja, kwa kuwa haifanyi kazi yoyote na kwamba, kukosekana kwake katika Bandari ya Dar es Salaam kunasababisha msongamano wa mizigo.
Maagizo hayo yalitolewa na Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa, Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene baada ya kufanya ziara fupi ya pamoja jana katika Bandari ya Dar es Salaam.
Wakati mawaziri hao wakitoa maagizo hayo, TPA ilieleza kuwa ili kuboresha huduma za bandari zote zilizopo nchini, inahitaji kupatiwa mkopo wa Dola 4 bilioni za Marekani.
Sakata la kunyofolewa kwa kipengele hicho cha mkataba, liliibuka baada ya Dk Mwakyembe kumbana Kaimu Mkurugenzi wa TPA, Madeni Kipande akieleza kwamba, licha ya mamlaka hiyo kukabidhiwa mtambo huo na mwekezaji ambaye ni Kampuni ya Leighton ya Singapore, inaonekana kuna kipengele ndani ya mkataba huo kimeondolewa.
“Awali mkataba ulieleza wazi kwamba baada ya kampuni hii kukamilisha kazi yake ya kuweka mtambo ingetuachia vifaa vya ukarabati wa mtambo ambavyo vina thamani ya Dola 300 milioni, lakini kampuni hii haikuacha, kwa nini” alihoji Dk Mwakyembe na kuongeza:
“Vifaa hivi vya ukarabati tungevitumia kwa muda wa miaka miwili, sasa tunataka kujua aliyekichomoa kipengele hiki ni nani, ili na sisi tumchomoe.”
Baada ya kauli hiyo ya Dk Mwakyembe, Simbachawene alizidi kumbana Kaimu Mkurugenzi huyo akisema: “Na kwa nini mkataba ubadilishwe wakati hicho kipengele ndiyo kilikuwa moja ya sababu za mwekezaji kupata hiyo zabuni ya ujenzi wa mtambo, hapa TPA si kuna wanasheria, iweje litokee hili?”
Akijibu swali hilo, Kipande alisema kuwa baada ya zabuni hiyo kupita kipengele hicho kiliondolewa, hivyo kuilazimu TPA kuingia gharama za kufanya matengenezo.
“Nilichokieleza ndiyo hicho… Ila naomba muda ili niliandike kwa maandishi suala hili,” alisema Kipande.
Licha ya maelezo hayo, Dk Mgimwa alimwambia Kipande kuwa wao wanahitaji taarifa sahihi ili wajue aliyekiondoa kipengele hicho kwa kuwa hali hiyo inaonyesha wazi kwamba bandari inahujumiwa, huku akiitika Bodi ya TPA kueleza hatua ilizochukua hadi sasa.
mwananchi

No comments:

Post a Comment