
 
Yapata
 wiki tatu sasa tangu msanii mwenzangu Steven Kanumba aage dunia, na 
kama ilivyo kwa kila kitu kinapotokea huandamana na kila aina ya maneno 
na hisia mbali mbali kutokana na mitazamo ya watu kupishana kuhusiana na
 jambo husika. Kulingana na muktadha huo, msiba wa Steven Kanumba 
umekumbwa na maneno na hisia kama hizo, hususan mazingira ya kifo chake;
 kinachosikitisha zaidi watu wengi (ambao wanajitambulisha kama wapenzi 
wa Kanumba), na baadhi ya vyombo binafsi vya habari vimekuwa 
vikinihusisha na kifo hicho, kwa kusema kwamba kwa njia moja au nyingine
 ninahusika na mauaji ya Steven Kanumba. Kwa muda wote huo tangu msiba 
ulipotokea mpaka leo hii nashika kalamu kujaribu kuyaweka sawa na 
kuondosha hisia chafu katika fikra za watu, nimekuwa nikipitia katika 
wakati mgumu sana kwa jinsi ambavyo nimekuwa nikinyooshewa vidole kila 
upande nikihusishwa na kifo hicho, kiujumla nimezingatia maoni ya 
wapenzi ya mashabiki wangu wakinitaka kuwa na subira,  ila
 kuna ukweli usemao kwamba, uongo ukirudiwa sana jamii huusadiki na 
kuuona ukweli, nimeona nisikae kimya ila niweke sawa hili kwamba 
sihusiki na kifo cha Steven Kanumba.
Nasema
 wazi kwanza sihusiki kabisa na kifo cha Kanumba kwanza kwa kuzingatia 
mazingira yenyewe ya kifo kilivyotokea. Wakati kifo hicho kinatokea, 
nilikuwa sehemu nyingine kabisa na mimi nilikuwa mtu wa tatu kutaarifiwa
 kwamba Kanumba amepatwa na mkasa ambao baadae ulisababisha kifo chake. 
Na na hata nilipofika katika hospitali ya Muhimbili (tofauti na watu 
wanavyodhani kuwa nilifika nyumbani kwake; ukweli mimi nilimkuta tayari 
amepelekwa Muhimbili), nilikuta tayari alikuwa ameshafariki ndio maana 
hata Polisi wanaohusika na usalama wa raia, si tu kwamba hawakuniweka 
chini ya ulinzi, sikuitwa hata kuhojiwa kwa sababu hakuna mazingira 
yoyote yanayonihusisha mimi na kifo hicho.
Pili,
 watu wanahusisha tofauti za kibinadamu zilizokuwepo baina yetu na kifo 
hicho, nasema hii sio sahihi kwa sababu kwanza ni kawaida kwa binadamu 
kutofautiana, isipokuwa kwetu sisi baadhi ya vyombo vya habari vilikuwa 
vinakuza kwa sababu nisizozijua, hivyo jamii ikachukulia kuwa tofauti 
zile ni uadui kitu ambacho sio sahihi, kwani sisi hatukuwa watu pekee 
tunaotofautiana kwani huu ni mwenendo wa kawaida wa dunia; hivi jana 
tumeshuhudia Waziri mmoja akieleza bayana katika mkutano na waandishi wa
 habari kuwa na tofauti na naibu wake, lakini hatuajasikia ikiandikwa 
wana ‘bifu’ bali imetafutwa lugha nzuri ya kupamba tofauti hizo, kwa 
kuwa waliohusika ni waheshimiwa, ila kwa wengine kutokana na sababu 
tusizozijua, inaonekana kama ni haki yetu kuandikwa vibaya. 
Kinachosikitisha, kwa nini jambo hili linachukuliwa kwa mkazo mkubwa 
sana, kwani hatujawahi kusikia watu wakiwa wanatofautiana na ndugu jamaa
 hata na marafiki zao na inaonekana kawaida tu? Kwani vyombo vya habari 
havikuwahi kuandika kuwa marehemu Steven Kanumba alikuwa na tofauti na 
baba yake, na yeye mwenyewe alitamka hivyo katika vyombo vya habari, 
mbona wameliongea bila kuongeza chumvi, na jamii inaona kuwa ni jambo la
 kawaida la kibinadamu.
Pengine
 watu wanaojaribu kuongea hayo, hawajui mimi na Steven Kanumba tumetoka 
wapi? Sisi si watu tuliokutana barabarani, tuna historia katika kazi 
yetu ya sanaa na pia katika maisha maisha yetu. Mwanzoni kabisa, mimi 
ndiye niliyempokea Kanumba pale Kaole na ndiye niliyemfundisha sanaa 
pale (nadhani watu wanakumbuka tamthiliya za wakati huo ITV) na baada ya
 hapo tulienda pamoja katika kampuni ya Game 1st Quality 
pamoja na tukafanya filamu kama Johari, Sikitiko Langu, Dangerous Disire
 na nyinginezo, na tuliendelea kuwa pamoja katika kampuni hiyo mpaka 
tulipofanya filamu ya Oprah mwaka 2008 ambapo niliingia rasmi kufanya 
kazi za kampuni yangu, lakini tuliendelea kuwa pamoja hata wakati 
nikiendelea na kazi za kampuni yangu. Pia mimi nilikuwa wa kwanza kuanza
 kufanya kazi na Steps na baadae Kanumba alipoanza kufanya kazi zake 
mwenyewe na kunikuta huko tuliendelea kuwa pamoja kama siku zote. Kitu 
kikubwa kilichokuwa kinaendelea baina yetu, ni kwamba tulijenga 
ushindani wa kuendeleza kazi mbele kwa kila mmoja akitoa kazi, mwingine 
anamjibu,  Isitoshe hata vitu 
vyetu binafsi utaona kama kuna kufanana; kuna wakati Kanumba alinunua 
Toyota Ruv 4 nyeusi mimi nikanunua ya kijani, aliponunua Harrier na mimi
 nikanunua pia, na hata gari za hivi karibuni, ukitazama utaona kuwa 
zinafana kwa karibu; hii ilikuwa ni kama maisha yetu, hatukuwa na uadui,
 ilikuwa tunapeana changamoto za maendeleo.
 Watu
 wanaojaribu kuonesha kuwa tofauti zetu ilikuwa ni uadui, huwa hawajui 
wapi tulikotoka ndio maana wanasema wasemavyo na katika kuthibitisha 
kuwa tofauti hizo hazikufikia katika uadui, kuna watu ambao wanafanya 
kazi nami katika kampuni yangu ya RJ ndio hao hao Kanumba alikuwa 
anawatumia siku zote katika kazi zake, hata baada ya tofauti hizo hakuna
 aliyekoma kufanya kazi na yeyote kati yetu. Hii inathibitisha kuwa 
tofauti ilikuwa kati yetu kama binadamu, sio chuki za kimafanikio, 
ingekuwa hivyo watu kama Junior Syaary ambaye mara nyingi hufanya final 
editing katika RJ ndio huyo huyo alikuwa akifanya na Kanumba, Ally 
Yakuti ambaye anaandika script za RJ, ndiye huyo huyo aliyekuwa 
anaandika kwa Kanumba, Steven Shoo ambaye ni mtaalamu wangu wa light, 
ndiye huyo huyo anayetumiwa na Kanumba na wengine wengi kama Juma 
Chikoka aliyecheza kikamilifu katika filamu ya kijiji cha Tambua Haki, 
ambaye pia anashiriki filamu nyingi za RJ, na wote hao, hawakuanzia kwa 
Kanumba, wote wameanza kwangu mimi ndio niliompatia na hata baada ya 
hayo yanayosemwa kuwa kuwa ni uadui, sikuwahi kuwakataza kufanya kazi na
 Kanumba.
Tatu
 kumtuhumu mtu kwa namna yoyote ile bila ya uthibitisho wa tuhuma hizo, 
ni kosa kwa sheria za nchi na pia kama ni mfuasi wa dini yoyote ni 
dhambi, kwani wakati ukisema hayo huku hujui uhalisia bali unasukumwa na
 nguvu za hisia tu ni sawa na kumchafua mtu huyo katika jamii bila ya 
kujua jamii inamchukuliaje. Napenda kusema wazi wazi kuwa, kwa kila 
anayetekwa na wimbi hili, ajaribu kufikiria leo ipo kwangu mimi, kesho 
inaweza kuhamia kwako, kwani mimi sio wa kwanza kufikwa na haya, inaweza
 kukukuta hata wewe au ndugu yako, utajisikiaje. 
Mwisho
 kabisa napenda kumaliza kwa msemo usemao, ajidhaniaye amesimama, 
aangalie asianguke, kwani kadri mambo haya yanavyoendelea, usidhani 
yataishia kwangu, kwani mkono wa dhuluma haushii karibu, ukisikia jirani
 anapiga kelele za mwizi, usilale kamsaidie, usiseme kuwa hatuhusiki 
kwani hayupo kwetu, kesho utafikwa na wewe utakosa wa kukusaidia. cha 
msingi kama tunampenda sana ndugu yetu ni kumuombea kwa Mungu, kwani 
hatujui makao yake huko aliko, na sio kuunda vitu ambavyo kamwe hata 
yeye angekuwa hai asingeviafiki.
MUNGU AILAZE ROHO YA MAREHEMU STEVEN KANUMBA MAHALI PEMA
 PEPONI
MUNGU IBARIKI AFRIKA MUNGU IBARIKI TANZANIA