Wednesday 18 April 2012

wengi matatani kifo cha kanumba



BADO sakata la kifo cha Steven Charles Kanumba ‘The Great’ ni bichi na kwa mambo yalivyo, kuna uwezekano watu wengi zaidi wakaingia matatani kwa namna moja au nyingine, Risasi Mchanganyiko limeshiba data.
Habari zinadai kuwa wakati upelelezi ukiendelea, kuna ambao tayari wamehojiwa na inawezekana wengi watahojiwa kwa kadiri ishu hiyo inavyozidi kuchukua sura mpya.

WALIOHOJIWA
LULU
Ukimwondoa mtuhumiwa namba moja wa kifo hicho, Elizabeth Michael ‘Lulu’, ambaye alishahojiwa na kupandishwa kizimbani kisha kuwekwa nyuma ya nondo za mahabusu ya Segerea, Dar, kuna wengine walio roho juu.

SETH BOSCO
Katika tukio hilo, pia tayari ndugu ambaye ni mdogo wa marehemu Kanumba, Seth Bosco naye alishafikishwa kwenye kituo cha polisi cha Oysterbay Kinondoni na kuhojiwa kuhusu anachokijua juu ya kifo hicho kwa kuwa ndiye mtu wa kwanza kuingia chumbani baada ya staa huyo kudondoka.

DAKTARI
Naye aliyekuwa daktari wa marehemu Kanumba aliyetajwa kwa jina moja ka Kabugi maarufu kama Kidume, alikuwa mmoja wa watu waliofika kituo cha polisi Oysterbay kutoa maelezo akiwemo mwigizaji swahiba wa marehemu Kanumba, Vincent Kigosi ‘Ray’.

RAY
Pamoja na kuwa mmoja wa watu waliokwenda kutoa maelezo polisi siku ya tukio la kifo cha Kanumba Aprili, 7, mwaka huu, mwishoni mwa wiki iliyopita Ray alizua gumzo baada ya kupamba ukurasa wa mbele wa gazeti moja litokalo kila siku akikanusha kuhusika na kifo hicho.
Swali kwa Ray lilikuwa ni nani aliyemwambia kuwa kahusika hadi akanushe hivyo kumjengea picha ya tofauti kwenye jamii.

ALI KIBA
Mwishoni mwa wiki iliyopita, staa wa Bongo Fleva, Ali Saleh Kiba, naye alisikika akikanusha kuwa si kweli kwamba alihojiwa juu ya sakata hilo kufuatia madai kuwa ndiye aliyempa lifti Lulu wakati anaondoka kwa Kanumba baada ya tukio hilo.

WENGI ZAIDI KUINGIA MATATANI
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kindoni, Charles Kenyela alipokuwa akifunga mjadala huo na kuachia Kitengo cha Upelelezi wa Makosa ya Jinai kifanye kazi yake, katika sakata hilo watu wengi watahojiwa kwani watafuatilia vyanzo mbalimbali ikiwemo simu za Kanumba na Lulu kujua watu waliowasiliana nao wahojiwe wanahusikaje na tukio hilo.

‘KUFA KUFAANA’ NAO MATATANI
Mbali na kesi ya mauaji ya Kanumba, pia waliotumia kifo cha Kanumba kujitajirisha (kufa kufaana) kwa kuchuuza bidhaa mbalimbali za msanii huyo mkubwa ndani na nje ya nchi, nao wameingia matatani kwa kukamatwa na kutiwa mbaroni.
Bidhaa ambazo zilipigwa marufuku kuuzwa na shirikisho la filamu nchini (TAFF) ni pamoja na nguo, vitabu na mikanda ya mazishi ya Kanumba hivyo kila aliyekamatwa na ‘prodakti’ hizo aliingia matatani.

GPL

No comments:

Post a Comment