Tuesday 29 May 2012

KAULI ZA VIONGOZI KUHUSU VURUGU ZANZIBAR




SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) imesema operesheni ya kuwasaka wahalifu walihusika na vurugu za wiki iiliyopita inaendelea na Serikali haitakuwa na msalia mtume kwa yeyote aliyehusika na vurugu hizo.

Akizungumza katika mkutano na viongozi wa dini katika ukumbi wa Kanisa la Pentekoste Tanzania lililopo Kariakoo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohammed Aboud Mohammed alisema Serikali imesikitishwa na kitendo kilichotokea cha vurugu na uchomaji wa nyumba za ibada, Makanisa.

“Hizi ni njama za makusudi, nataka nisemawazi kwamba watu hawa wametangaza mapambano na Serikali,tutawashughulikia ipasavyo,” alionya Waziri Aboud.

Watu waliofanya vurugu Zanzibar sasa watakiona kwani wametangaza mapambano na Serikali, itawashughuliki popote walipo.

Waziri Aboud alisema kwamba waumini wa dini zote wamekuwa wakiishi kwa upendo na maelewano makubwa kwa miaka mingi ambapo ustahamilivu wa kidini upo kwa hali ya juu katika Visiwa vya Unguja na Pemba.

“Mie nakumbuka nilipokuwa nakaa kule Shangani kwa mfano Mwezi wa Ramadhani utakuta tunapelekeana vyakula, waislamu wanapeleka kwa wakristo na hata siku ya sikuuu ya Idd el Fitr tunasherehekea pamoja, huwezi kubagua yupi mkristo yupi Muislam,” alisema waziri hyo.

Alisema Serikali inawapo pole waumini wa makanisa yaliyochomwa moto na kuwaahidi hatua kali zitachukuliwa dhidi ya wale wote waliohusika.

Akizungumza katika mkutano huo,Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali Said Mwema alisema Polisi imejipanga kimkakati kukabuiliana na wale wote watakaofanya au kuchochea ghasia.

“Tunaendelea kudhibiti hali,doria kama kawaida na pia tumeweka ulinzi maalum katika nyumba za ibada tumezijumuisha katika sehemu muhimu za ulinzi kwa kipindi hichi,” alisema IGP Mwema.

IGP Mwema alisema pia ameunda timu maalum ya kikosi kazi ambacho kinajumuisha maafisa kutoka Idara ya Upelelezi Makao Makuu Dar es Salaam kuchunguza matukio ya vurugu hizo na kuwachukulia hatua watakaobainika.

Alisema katika mkutano huo pia jumla ya watu 46 wamekamatwa jana (juzi) na kati ya hao 43 wamefikishwa mahakamani jana Mjini Zanzibar wakikabiliwa na tuhuma mbalimbali.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Abdallah Mwinyi Khamis alisema Serikali ya Mkoa wake imesikitishwa mno na vitendo vya ghasia na uchomaji wa makanisa moto.

Mkuu huyo wa Mkoa alisema uvumilivu wa kidini ni jambo la msingi sana na anaamini waliofanya vurugu na kuchoma baadhi ya makanisa moto sio waumini wa dini ya Kiislamu bali ni wahalifu.

“Tujiulize jamani, hivi kweli muumini wa kiislam anaweza kwenda kuvunja baa na kasha kuanza kunywa pombe? Hawa sio Waislam …hapa kuna jambo, tutawachunguza kubaini chanzo na wanaohusika na kadhiaa hii,” alisema Mkuu huyo wa Mkoa.

Akithibitisha uvumilivu wa kidini uliokuwepo Zanzibar tangu enzi na enzi, Mkuu wa Mkoa alitoa Stempu ya Serikali ya Kikoloni iliyopambwa kwa picha za misikiti na makanisa wakati wa utawala wa Kisultani chini ya himaya ya Uingereza yenye ujumbe wa uvumilivu wa kidini Zanzibar.

“Stempu hii iliyokuwa imetolewa na Serikali ya Kiingereza wakati ule inathibitisha kwamba Zanzibar hakuna tatizo la waislamu na wakristo,huu jamani ni ushahidi tunashangaa leo wanatoka watu wanachoma moto kanisa,” alisema.

Alitoa mfano wa namna wananchi Zanzibar walivyokuwa wakiishi kwa upendo na mshikamano wa maziko ya aliyekuwa Waziri Mwandamizi katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, marehemu Brigedia Jenerali Adam Mwakanjuki, idadi ya Waislamu mazikoni ilikuwa kubwa kuliko ya dini nyingine.

“Mbali na hili la mwenzetu Mwakanjuki, mimi mwenyewe niliombwa na Skuli ya Kanisa St Joseph kusomesha, walikuwa na upungufu wa walimu, Wizara ya Elimu ikaniteuwa mie nienda kusomesha, nimeishi nao vizuri, hawakunitenga …mimi ndio mwalimu wa mwanzo muislam kusomesha skuli ya wakristo hapa Zanzibar,” aliongeza Mkuu huyo wa Mkoa.

Katibu Mkuu wa Makanisa ya Pentekoste Tanzania, Askofu David Mwasota aliishukuru Serikali kwa kuwaunga mkono na kuwa pamoja nao kitendo ambacho kinathibitisha dhamira njema ya Serikali na viongozi kwa ujumla.

Askofu Mwasota alisema kesho (leo) watafanya mkutano wa madhehebu yote ya kidini kuzungumzia kadhia hiyo mkutano ambao utafanyika katika Kanisa la Pentekoste Kariakoo Unguja.

Mkuu wa Dini ya Kiislam katika Ofisi ya Mufti Mkuu Zanzibar, SheikhThabit Noman Jongo ameshangazwa na watu wanaochoma moto makanisa na kuwafananisha watu hao kuwa ni wahalifu na Serikali iwachukuli hatua kali kwani Waislam hawana ugomvi na Wakristo.
 
 Na Juma Mohammed – MAELEZO, Zanzibar

No comments:

Post a Comment