Wednesday 9 May 2012

KIMA CHA CHINI SASA KUWA 180,000/=!


0diggsdigg
NI BAADA YA MAJADILIANO YA SERIKALI NA TUCTA
Waandishi Wetu
KUNA taarifa kwamba Serikali imekubali kuongeza mishahara kwa watumishi wa umma kwa kati ya asilimia 20 na 33.3 katika Bajeti ya mwaka wa fedha wa 2012/13.Hatua hiyo inamaanisha kwamba kima cha chini cha mshahara sasa kitakuwa kati ya Sh180,000 hadi Sh200,000 kutoka Sh150,000 zinazolipwa sasa.Vyanzo vya habari kutoka serikalini vimeeleza kwamba nyongeza hiyo ya kati ya Sh30,000 hadi Sh50,000 ni matokeo ya mazungumzo kati ya Serikali na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta).Mbali ya kutaja kima hicho, vyanzo hivyo vimeeleza kuwa nyongeza hiyo inaweza kuvuka Sh50,000 kutegemea uwezo wa Serikali.

Hata hivyo, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma), George Yambesi alipoulizwa kuhusiana na taarifa hiyo alijibu kwa kifupi kuwa hakuwa katika nafasi ya kuzungumzia hilo.

“Sipo katika ‘position’ (nafasi) nzuri ya  kuzungumzia hilo, nadhani suala la mishahara. Mheshimiwa Rais alishalizungumzia kwenye hotuba yake ya Sikukuu ya Wafanyakazi,” alisema.

Katika hotuba yake kwenye kilele cha sherehe hizo zilizofanyika kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga, Rais Jakaya Kikwete alisema Serikali inatambua mazingira magumu ya kazi waliyonayo wafanyakazi na kwamba ipo tayari kuyaboresha.

Alisema imesikia madai ya wafanyakazi na itaendelea kuyafanyia kazi. Madai aliyoahidi kuyafanyia kazi ni pamoja na kupunguziwa kodi ya mapato.

Kwa upande wa Tucta, Katibu Mkuu wa Shirikisho hilo, Nicolaus Mgaya alipoulizwa jana alisema hajui Serikali itaongeza mshahara kwa kiasi gani lakini akasema anaamini kuwa ni sikivu.

Alisema kwa miaka mingi wafanyakazi wamekuwa wakilalamikia mishahara midogo ambayo haikidhi mahitaji, jambo ambalo limesababisha kuwepo kwa migongano ya hapa na pale na Serikali akasema kutokana na hali hiyo, wanaamini kuwa wataongezewa.

“Tunaamini linaweza kutekelezeka (suala la kuongezewa mishahara), lakini hakuna anayejua nyongeza hiyo itakuwa ni kiasi gani, kwa hiyo ukinitajia kiwango nashindwa kuelewa umekitoa wapi,” alisema Mgaya alipoulizwa kama nyongeza hiyo ni kati ya Sh30,000 na 50,000.

Mgaya alisema mbali na kuomba nyongeza mshahara, Tucta pia imeiomba Serikali kupunguza gharama za tozo za mifuko ya hifadhi ya jamii huku ikienda pamoja na udhibiti wa mfumuko wa bei ambao umekuwa kikwazo kwa wafanyakazi na kuwafanya kuishi katika mazingira magumu kiasi cha kushindwa kujituma ipasavyo na wengine kukimbilia kwenye sekta binafsi.

“Wafanyakazi ni tabaka kubwa, lakini limesahaulika. Hii inatokana na Serikali kushindwa kusikiliza kilio chao cha kuwaongezea mishahara jambo ambalo limechangia kulipwa ujira mdogo na kusababisha wengi wao kukimbilia kwenye sekta binafsi, kutokana na hali hiyo tunaamini kuwa Serikali itasikilia kilio chetu,” alisema.

Madai ya wafanyakazi

Sakata la mshahara wa wafanyakazi liliibua mgogoro mkubwa baina ya Serikali na Tucta na mwaka 2010, Shirikisho hilo liligoma kumwalika Rais Kikwete kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya Mei Mosi kitaifa kama ilivyokuwa utamaduni wake.

Hatua hiyo ya Tucta ilitokana na kile lilichodai kuwa Serikali siyo sikivu na lilitumia siku hiyo kujadili na kutoa tamko la kuitaka kutangaza kima kipya cha mshahara cha Sh315,000 ndani ya siku mbili la sivyo wafanyakazi wa umma wangeingia katika mgomo nchi nzima.

Hatua hiyo ilimlazimu Rais Kikwete kuitisha mkutano na Wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam Mei 3, 2010 na kujibu hoja mbalimbali za Tucta na kuweka msimamo wa Serikali kuwa haiwezi kulipa kiasi hicho cha fedha.

Rais Kikwete aliwatuhumu viongozi wa Tucta kuwa ni waongo na kwamba walikuwa hawasemi ukweli juu ya kile walichokuwa wanabaliana katika vikao vyake na Serikali.

Alisema Serikali ikifanya kima cha chini kuwa Sh300,000 kwa watumishi wa umma, itabidi iwalipe Sh6.9 trilioni kwa mwaka wakati makadirio ya makusanyo ya mapato ya Serikali kwa mwaka 2010/11 ni Sh5.8 trilioni.

CHANZO:MWANANCHI

No comments:

Post a Comment