Thursday 15 December 2011

jokate amburuza wema mahakamani kwa kumsingizia kuiba mchumba


NI vurugu mechi kati ya Miss Tanzania 2006, Wema Sepetu (pichani) na namba mbili wake, Jokate Mwegelo, mtifuano ni mzito lakini habari mpya ni kwamba sakata hilo linahamia kwenye mkondo wa kisheria.
Wema anamtuhumu Jokate kutoka kimapenzi na aliyekuwa mchumba wake, Naseeb Abdul ‘Diamond’, kitu ambacho kimesababisha wamwagane.
Kwa mujibu wa rafiki wa Jokate, Wema atasimamishwa kortini siku chache zijazo kujibu tuhuma za kumchafua mrembo huyo.
Rafiki huyo aliyeomba hifadhi ya jina lake gazeti alisema, Jokate yupo kwenye mazungumzo na mawakili watatu wazito nchini ambao ndiyo watakaosimamia kesi hiyo.
“Jokate ameumizwa sana na tuhuma za Wema, anasingiziwa bila hatia. Ameona hakuna sehemu ambayo anaweza kupata haki yake zaidi ya mahakamani.

“Anajadiliana na mawakili wake jinsi ya kumfungulia civil case (kesi ya madai),” alisema rafiki huyo wa Jokate kisha akaongeza:
“Mwanzoni Jokate alitaka ampuuze Wema, azungumze mpaka yaishe lakini mashambulizi ya Wema ni makali na yanamchafua. Jokate siyo aina ya wanawake mastaa wanaoweza kuvumilia skendo za vyombo vya habari.

“Yule Jokate ni staa mwenye malengo ndiyo maana hataki kuona heshima yake inavunjwa kwa mtindo huu. Na kwa hali ilivyo, sidhani kama Wema anaweza kupona, wale mawakili ni hatari sana.

“Tunajua Wema amezoea kesi lakini hii ya sasa ni nzito. Jokate anataka jamii imuone hana hatia kwa kumfundisha adabu Wema kutokana na maneno yake anayomchafua.”

Rafiki huyo wa Jokate alisema kuwa ‘shosti’ wake amewatuliza wazazi wake na ndugu wengine katika familia yake kwamba skendo ya kutoka na Diamond siyo ya kweli, hivyo amepewa shinikizo la kumshughulikia Wema.

“Hili jambo siyo mchezo hata kidogo. Wema ana kesi nzito kwa sababu hana uthibitisho wa tuhuma anazotoa kuhusu Jokate kutembea na Diamond. Anazungumza tu bila mpangilio.

“Ingewezekana Jokate kuzungumza na waandishi wa habari kuhusu kesi yake lakini hataki kabisa kufanya hivyo. Wema anazungumza na vyombo vya habari, sasa anaona na yeye akizungumza na vyombo vya habari itakuwa kuzidi kukuza mjadala na kumpa kichwa Wema.

“Kwa jinsi mambo yanavyokwenda, bila shaka ndani ya kipindi kifupi kesi itakuwa imeshasajiliwa mahakamani na Wema ataitwa kwa ajili ya kusimamishwa kizimbani kujibu tuhuma za kumchafua Jokate,” alisema.

KILICHOMUUDHI ZAIDI JOKATE
Rafiki huyo alisema kuwa kitu ambacho kilimuudhi zaidi Jokate ni matamshi ya Wema ‘aliyomshuti’ kupitia kwenye redio moja nchini Jumatatu iliyopita.

Inaelezwa kuwa Wema alimponda Jokate kuwa ni ‘mdada’ anayejifanya mlokole, anajiheshimu na muimba kwaya, kumbe anachukua wapenzi wa watu.

NENO LA WEMA
Wema akizungumza na paparazi wetu, alisema kuwa ameondoka kwa Diamond baada ya kujiridhisha kwa ushahidi wa kina kwamba anatoka na Jokate.

Mrembo huyo huyo alisema, anaumia kwa sababu aliamua kutulia na Diamond kwa mapenzi yote na uaminifu, kumbe mwenzake hakuwa na utulivu.

“Unajua watu wengi wanajua mimi situlii na mwanaume mmoja kitu ambacho nakipinga kabisa, kwa maana kuna wakati navumilia ninayofanyiwa na wanaume lakini inashindikana, ushahidi ninao kwamba Diamond ametembea na Jokate,” alisema Wema.

JOKATE
Kwa upande wake, alipozungumza na gazeti hili alisema kuwa hajawahi kuwa na uhusiano na Diamond kisha akaongeza:
“Sipendi matatizo na watu. Labda ameamua safari hii apambe vyombo vya habari na mimi. Diamond nilikuwa naye kikazi, mimi nimecheza video ya wimbo wake mpya unaoitwa Mawazo. Kama kuna maeneo tulikuwa pamoja ni kwa sababu za kikazi.”

Kuhusu kwenda mahakamani, Jokate alikataa kuzungumza chochote, kitu ambacho kilishabihiana na maneno ya rafiki yake kwamba mrembo huyo hapendi kuzungumza mambo hayo kwenye vyombo vya habari.

chanzo>>:amani

No comments:

Post a Comment