Friday 9 December 2011

KILI STARS CHALII



KUNA msemo wa Kiswahili kuwa ‘kutangulia siyo kufika’, hicho ndicho kilichotokea jana kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, pale timu ya taifa ya Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars, ilipoanza kufunga bao lakini ikajikuta ikiambulia kipigo cha mabao 3-1 kutoka kwa Uganda, The Cranes.

Kipingo hicho katika robo fainali kilihitimisha safari ya Kili Stars kwenye michuano ya Chalenji 2011, huku Uganda ikitinga fainali hiyo ambapo itakipiga dhidi ya Rwanda kesho kwenye uwanja huo.

Kocha wa Kili Stars, Charles Mkwasa, alitupia lawama zake kwa wachezaji wa Uganda ambao alidai walikuwa wakicheza rafu kiasi cha kusababisha wachezaji wake wengi kuumia.

Kiungo mshambuliaji Mrisho Ngassa ndiye alianza kuifungia Kili Stars katika dakika ya 17, Uganda ikasawazisha kupitia kwa Andrew Mwesigwa, matokeo yaliyodumu mpaka dakika ya 90. 

Baada ya kuongezwa dakika 30 ndipo Kili Stars ilipoteza mwelekeo na kujikuta ikipigwa mabao mawili wafungaji wakiwa Emmanuel Okwi (111) na Isaac Isinde (112) ambaye alifunga kwa penalti. 

Katika mechi ya kwanza, Rwanda iliifunga Sudan mabao 2-1.

Kutokana na matokeo hayo, Uganda itakipiga dhidi ya Rwanda, huku Kili Stars ikicheza dhidi ya Sudan kesho saa nane kutafuta mshindi wa tatu.


source:GPL

No comments:

Post a Comment