Sunday 26 August 2012

NAPE KUSHTAKIWA NA CHADEMA KWA KAULI ZAKE


Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimeanza kuchukua hatua za kisheria dhidi ya Nape Nnauye Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM kufuatia madai ya uzushi na uongo aliyoyatoa tarehe 12 Agosti 2012 kuwa anao ushahidi kwamba CHADEMA kimekuwa kikiwahadaa wananchi kwa kuwachangisha fedha huku kikipokea mabilioni ya fedha kutoka kwa wafadhili kutoka nje.
Izingatiwe kuwa matamshi yake yalitangazwa na vyombo vya habari vya kielektroniki ikiwemo vituo vya televisheni, radio na kusambazwa kwenye mitandao ya kijamii tarehe 12 Agosti 2012 na katika kurasa za mbele za magazeti mbalimbali tarehe 13 Agosti 2012.
Bodi ya Wadhamini wa CHADEMA iliagiza wanasheria wamwandikie barua ya kumtaka kukiomba radhi Chama Cha Demokrasia na Maendeleo kwa kutumia njia ile ile aliyotumia kufanya propaganda chafu za kuikashifu na kuifitisha CHADEMA kwa umma wa watanzania ikiwemo kuzusha kuwa upo uwezekano wa CHADEMA kupewa fedha hizo kwa mikataba yenye masharti ya kuiweka nchi rehani.


Tayari ameshaandikiwa barua ya kisheria tarehe 24 Agosti 2012 ya kumtaka aombe radhi na kulipa fidia ya bilioni tatu kwa matamshi hayo ya uzushi na uongo yenye maana ya kuwapotosha waliyoyasikia na kuyasoma kuwa CHADEMA kinawalaghai wananchi, kina viongozi wasio waaminifu na kwamba kiko tayari kuuza nchi wa uroho wa madaraka.

Kipaumbele cha CHADEMA katika suala hili ni kuombwa radhi hata hivyo kiwango cha fidia ya fedha kwa fedheha kilichotakiwa ni fundisho kuwa uzushi na uongo unagharimu.

\Ikumbukwe kwamba tarehe 12 Agosti 2012 nilitoa kauli ya awali baada ya mkutano Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM na waandishi wa habari ambapo pamoja na mambo mengine nilieleza kwamba tutatoa tamko la kueleza hatua za ziada baada ya kupata taarifa kamili aliyoitoa.



Katika kauli hiyo nilitoa mwito kwa Mwenyekiti wa CCM Rais Jakaya Kikwete kueleza watanzania iwapo propaganda hizo chafu zina baraka zake; hivyo ukimya wake mpaka sasa kuhusu matamshi hayo inakifanya CHADEMA kuwa na imani yenye shaka (benefit of doubt) kwamba Nape hakutumwa na chama chake kutoa matamshi aliyoyatoa.

CHADEMA inachukua fursa hii kuutaarifu umma kwamba asipotekeleza matakwa hayo ndani ya siku saba kuanzia tarehe hiyo aliyopokea barua hatua nyingine ya kumfikisha mahakama kuu zitaanzishwa ili aweze kuchukuliwa hatua zaidi.
Pamoja na kuchukua hatua za kisheria, CHADEMA kinaendelea kutimiza dhima yake ya kuleta uongozi bora, sera sahihi, mikakati makini na oganizesheni thabiti kwa maendeleo endelevu ya Tanzania kwa pamoja na mikakati mingine kutekeleza operesheni ya vuguvugu la mabadiliko nchini (M4C) na tunawashukuru wananchi kwa kuendelea kuunganisha nguvu ya umma kwa hali na mali katika maeneo mbalimbali nchini.
Imetolewa tarehe 26 Agosti 2012 na:
John Mnyika (Mb)
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi

No comments:

Post a Comment