Saturday 25 August 2012

PAPAA MSOFE GONJWA GONJWA


Marehemu Chasphori Kituli
Stori: Richard Bukos
MFANYABIASHARA maarufu jijini Dar es Salaam, Abubakar Marijani ‘Papaa Msofe’ ameripotiwa kuwa na hali mbaya gerezani kufuatia kukabiliwa na maradhi.
Taarifa hiyo ilitolewa na Mwendesha Mashitaka wa Serikali, Mwanaisha Komba wakati akimuomba Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, jijini Dar es Salaam, Agnes Mchome, kuahirisha kesi ya mauaji inayomkabili mshitakiwa huyo.
 Mwendesha mashitaka huyo alisema amepokea hati maalum kutoka Gereza la Keko, Dar anakoshikiliwa Papaa Msofe inayoeleza kuwa hali yake ni mbaya na asingeweza kufika mahakamani hapo.
Mwanahabari wetu alizungumza na mwendesha mashitaka huyo kutaka kujua zaidi kinachomsumbua mshitakiwa huyo lakini alisema kuwa taarifa alizopewa kutoka kwa afisa wa gereza hilo ni kwamba mshitakiwa ana hali mbaya hivyo asingeweza kufika mahakamani.
Mwanahabari wetu alizungumza na mmoja wa maofisa wa gereza hilo ambaye alidai matatizo yanayomkabili mshitakiwa ni mchafuko wa hali ya hewa, msongo wa mawazo na kutozoea mazingira ya gerezani.
“Si unajua hali ya gerezani? Kinachowaumiza wengi wakiwa kule ni msongo wa mawazo, kutojua hatima ya kesi zao na kutoyazoea mazingira,” alisema afisa huyo ambaye hakutaka kutaja jina lake kwa kuwa si msemaji wa jeshi hilo.
Kesi hiyo imeahirishwa mpaka Septemba 5, mwaka huu itakapotajwa tena mahakamani hapo.
Papaa Msofe anatuhumiwa kuhusika na mauaji ya mfanyabiashara Chasphori Kituli yaliyofanyika Magomeni Mapipa jijini Dar es Salaam

chanzo.GPL

No comments:

Post a Comment