Wednesday 5 September 2012

DIAMOND AFANYA KUFURU MAREKANI




STAA bei mbaya wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul Jumaa ‘Diamond Platnumz’ ameandika historia huko Washngton DC nchini Marekani kwa Rais Barack Obama baada ya kuangusha shoo iliyojaa kufuru na kupagawisha Wabongo na watu wa Afrika Mashariki waishio humo.
Tukio hilo lilijiri Jumapili ya Septemba 2, mwaka huu ambapo Diamond na ‘madensa’ wake watatu walikonga nyoyo za mashabiki wake waishio jijini humo na wengine kutoka katika miji jirani kama New York.
Akiwa stejini, Rais huyo wa Wasafi aligonga nyimbo zote za zamani na sasa na alipoona bado mashabiki wake wana mzuka aliwadondoshea ngoma mpya ambazo hata hajaziachia kwenye redio na televisheni za Kibongo.
Katika shoo hiyo iliyomtangaza kivingine katika Bara la Amerika, walioonekana kupagawa zaidi ni warembo na wake za watu ambao walishindwa kuvumilia na kujikuta wakikwea stejini na kumlowanisha na ‘madolari’ hivyo kuchafua jukwaa kwa manoti.
Kabla ya shoo, Diamond alipanda stejini akiwa ametupia ‘kibishoo’ lakini baada ya shoo kukolea, alichojoa viwalo vya juu na kubaki na ‘singilendi’ pekee hivyo kuwaacha watoto wazuri wa kike wakisema, “OMG (Ooh My God).”
Hata baada ya shoo kumalizika, baadhi ya mashabiki walitaka aendelee lakini muda haukumruhusu hivyo wakaondoka ukumbini kwa shingo upande kwani waliona walikatiziwa uhondo wa kuendelea na burudani kutoka kwa Diamond.
Kesho yake (Jumatatu), Diamond alisema: “Asante Mungu, nilifika salama DC (Washngton) nashukuru kwa kila jambo na hivi ndivyo tunavyofanya.”
Diamond alisema maneno hayo na kutundika picha kwenye mtandao wake zikimuonesha akiwa na madensa wake wakipata kifungua kinywa, akiwa ‘gym’ na baadaye wakiwa kwenye bwawa wakijiachia kwa kuogelea.

GPL

No comments:

Post a Comment